Friday, August 7, 2020

Watu wanne wakiwemo wakenya wawili wamefikishwa mahakamani kwa Uhujumu uchumi

RAIA wawili wa Kenya na Watanzania wawili, wamefikishwa katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu wakikabiliwa na mashitaka ya uhujumu uchumi ikiwemo kuisababisha Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA), hasara ya Sh milioni 16.6.

Washitakiwa hao ni Beth Ngunyi (43) mfanyabiashara na Mkazi wa Kasaram Nairobi, Frolence Dirango (34) mfanyakazi wa Kampuni ya Betlee kama Ofisa wa Teknolojia ya Habari na Mawasiliano, Alven Swai (26) mkazi wa Mbezi Beach na Godluck Macha (28) mfanyabiashara na Mkazi wa Mbezi beach.

Wakili wa Serikali, Batilda Mushi alidai mbele ya Hakimu Mkazi Mkuu, Yusto Ruboroga alidai kuwa kati ya Julai Mosi na Julai 26, mwaka huu katika maeneo mbalimbali, washitakiwa kwa pamoja walikula njama ya kutumia vifaa vya mawasiliano.

Alidai Julai 13, mwaka huu maeneo ya Tarakea wilayani Rombo mkoani Kilimanjaro, Ngunyi na Dirangu waliingiza vifaa vya kielekroniki nchini pasipo kuwa na leseni ya TCRA.
Mushi alidai Julai 20, mwaka huu maeneo ya Kibona Lodge Mbezi Beach jijini Dar es Salaam, washitakiwa hao walisimika vifaa vya mawasiliano bila kuwa na leseni kutoka TCRA.

Katika mashitaka ya nne, inadaiwa kati ya Julai 20 na 26, mwaka huu maeneo ya Kibona lodge Mbezi beach, kinyume na sheria walifanyia marekebisho ya vifaa hivyo vya kielektroniki.

Pia inadaiwa kinyume na sheria washitakiwa hao waliendesha mitambo ya mawasiliano bila kuwa na leseni.
Mushi alidai kinyume na sheria washitakiwa hao walitumia vifaa vya mawasiliano vilivyounganishwa na vifaa vingine vya mawasiliano kwa nia ya kupokea na kusambaza mawasiliano bila kupata uthibitisho wa TCRA.

Washitakiwa hao wanadaiwa walikwepa kufanya malipo ambayo yalipaswa kufanyika kwa kuruhusu mawasiliano nje ya nchi kutokana na kutumia kifaa hicho cha mawasiliano bila kuwa na leseni.

Katika mashitaka ya tisa, inadaiwa Julai 13, mwaka huu maeneo ya Kibona Lodge, Mbezi beach, washitakiwa Ngunyi na Dirangu wanadaiwa kuwepo nchini bila kuwa na kibali.

Mshitakiwa Macha anadaiwa Julai 15, mwaka huu kinyume na sheria aliwahifadhi Ngunyi na Dirangu kuishi kwenye Jamhuri ya Muungano wa Tanzania wakati wakijua hawana kibali.
Katika mashitaka ya 11, inadaiwa kati ya Julai 20 na 26, mwaka huu maeneo ya Kibona lodge Mbezi beach jijini Dar es Salaam washitakiwa hao waliisababishia TCRA hasara ya Sh 16,634,400.

Washitakiwa hao hawakutakiwa kujibu chochote kwa sababu mahakama hiyo haina mamlaka ya kusikiliza kesi za uhujumu uchumi.

Upande wa mashitaka ulidai upelelezi wa kesi hiyo bado haujakamilika na kuomba tarehe nyingine kwa ajili ya kutajwa.

Hakimu Ruboroga aliahirisha kesi hiyo hadi Agosti 20 mwaka huu kwa ajili ya kutajwa na washitakiwa wote wamerudishwa rumande kwa sababu mashitaka hayo hayana dhamana labda watakapoomba Mahakama Kuu.



source http://www.bongoleo.com/2020/08/07/watu-wanne-wakiwemo-wakenya-wawili-wamefikishwa-mahakamani-kwa-uhujumu-uchumi/

No comments:

Post a Comment